Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Philip Mangula amewaasa wananchi mkoani Njombe kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi ya kuwaua watu wanaotuhumiwa kufanya mauaji ya watoto mkoani humo.

Ametoa wito huo wakati akizungumza na viongozi wa CCM kutoka wilaya zote za mkoa wa Njombe pamoja na viongozi wa chama hicho ngazi ya mkoa mkutano uliofanyika Makambako wenye lengo la kutoa pole kwa viongozi, wanachama na wananchi mkoani humo.

Amesema kuwa miongoni mwa majukumu makubwa ya chama cha mapinduzi ni kulinda uhai wa raia wote wa Tanzania hivyo aliposikia uwepo wa matukio hayo ya mauaji ya watoto wadogo akiwa mkoani Mbeya kwa ziara ya kikazi aliamua kupita mkoani humo kutoa salamu za pole.

‘’Ndugu zangu wanachama na viongozi wa CCM naomba tuendelee kuelimishana ili tusichukue sheria mkononi maana tutakuwa tunapoteza kabisa ushahidi ambao huenda ungetusaidia kuwanasa wahalifu wanaofanya ukatili huu kwa watoto wetu na kuchafua hali ya mkoa wetu wa Njombe,’’amesema Mangula

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Njombe, Christopher Ole Sendeka amesema kuwa kwasasa hali ya usalama imeimarika kutokana na vyombo vya Ulinzi na usalama mkoani humo kuendesha Oparesheni maalumu iliyosaidia kukamatwa kwa baadhi ya wahusika.

Naye mwenyekiti wa CCM mkoa wa Njombe, Jassel Mwamwala amepongeza hatua zilizochukuliwa na serikali mkoani humo chini ya mkuu wa mkoa wa Njombe pamoja na kamati yake ya ulinzi na usalama na kusema kuwa jitihada hizo ziendelee hadi hapo wahusika wote wa mtandao huo wa uhalifu watakapotiwa mbaroni.

Wajasiliamali Dodoma waipa siku 14 Halmashauri kuzuia magari ya mizigo
Masilingi, Lissu ngoma mbichi, 'Ni bora urudi Tanzania ukasaidie upelelezi'