Katika harakati za kuboresha mazingira bora ya walimu kufanya kazi ili kuwawezesha kutoa elimu bora, leo Ubalozi wa China umemzawadia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, majengo matano ya kisasa kwa ajili ya ofisi za walimu.

Zawadi hiyo imekabidhiwa na balozi wa China, Wang ke ambaye amesema kwa miaka mitatu aliyoishi hapa nchini tangu alipoteuliwa kuwa balozi ameshuhudia maendeleo makubwa ya mkoa huo, hivyo wameona wasikae kimya kwenye jambo linalolenga kuleta ukombozi wa uchumi kupitia elimu.

Makonda ametangaza kuwa majengo hayo yatajengwa kwenye wilaya tano za mkoa wa Dar es salaam.

Leo Makonda ameweka jiwe la msingi pamoja na kukabidhi ramani ya jengo kuashiria kuanza kwa ujenzi huo kwenye shule ya sekondari Makumbusho.

Akiushukuru Ubalozi huo, Makonda amesema ujenzi wa majengo hayo kwa kiasi kikubwa unaenda kupunguza mateso ya walimu kufanya kazi katika mazingira magumu ikiwemo kufanya kazi kwenye madarasa.

Majengo hayo yanatarajiwa kuwa na Ofisi ya Mwalimu Mkuu, Mwalimu mkuu msaidizi, Ofisi ya walimu wote, ukumbi wa mikutano, chumba cha kuhifadhi mitihani, vifaa vya michezo, chumba cha muhasibu, chumba cha kubadili nguo, mapokezi, vyoo, bafu ikiwa na samani za kutosha.

Video: Kamanda Musilimu kula sahani moja na waegesha magari
Video: Ndomba amfunda Meja Jenerali Yakubu