Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amesema kuna gazeti moja nchini limekuwa likiandika habari za kumchonganisha yeye na viongozi wengine au taasisi nyingine za serikali, jambo ambalo amesema halikubaliki wala hawezi kulifumbia macho.

“Kuna gazeti moja linahangaika sana kuandika vitu vibaya kuhusu Mkoa wa Dar, wanajifanya wanajua sana sheria, wanachonganisha, na leo nimeona wameandika tena, wasitupotezee muda.

“Aliyeanza kugombanisha duniani ni shetani, lakini ilifika wakati akashindwa, hili gazeti raha yao wanataka wasikie mahakama imemkataa Mkuu wa Mkoa, hawaoni mateso ya wananchi wala kuyaripoti.

“Sasa aelewe tu kwamba hawatafanikiwa, nimeangalia nikabaini kuna ardhi moja bosi wao aliichukuaga, ipo tu limebaki poli katika eneo moja katika Wilaya ya Ubungo, tutaangalia taratibu angalau tuwapatie watu lijengwe soko la kisasa pale,” alisema Makonda bila kutaja ni gazeti gani.

Makonda ameyasema hayo jana, Feb. 14, 2018 wakati wa uzinduzi wa Jengo la Huduma za Mama na Mtoto katika Hospitali ya Amana, iliyopo Ilala jijini Dar ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Sababu za kuchoma vifaranga kutoka Kenya zawekwa wazi
Video: Dkt. Tulia afunguka mazito kuhusu matibabu ya Lissu