Mmiliki wa kituo cha E-FM/TV, Francis Siza maarufu kama Majizzo ameeleza jinsi alivyofanikiwa kumsajili kwenye kituo chake mtangazaji Jonijoo aliyekuwa anafanya kipindi cha Block 89 cha Wasafi FM na Bar Tender cha Wasafi TV.

Majizzo amesawazisha mlima wa kitendawili uliokuwa umeibuka kwenye mitandao ya kijamii, hasa baada ya kuweka kipande cha video kinachowaonesha baadhi ya viongozi wa E-Fm wakimtoa Jonijo jela, video iliyopata tafsiri nyingi kutoka kwa wadau wa kiwanda cha burudani.

Akizungumza kwa njia ya simu na SnS, Majizzo amesema alikuwa amepanga kufanya kazi na mtangazaji huyo tangu alipokuwa Times Fm, kituo ambacho kilimpa umaarufu na kumuweka kwenye kurasa za mbele za watangazaji wanaofuatiliwa kwa wakati huo.

Mmiliki huyo wa E-FM alieleza kuwa hakumchukua Jonijoo kama kulipa kisasi baada ya Wasafi kuichukua timu yake ya kipindi cha michezo, bali ulikuwa mpango wa muda mrefu ambao uliingiliwa na Wasafi.

“Jonijoo ni kijana ambaye mimi namkubali sana tangu akiwa kwa rafiki yangu Rehure [Nyaulawa] kule Times FM; na harakati za kufanya naye kazi tulizianza tangu kipindi hicho. Tulifikia sehemu nzuri tu, kwa bahati mbaya mimi nikasafiri, ilikuwa nikirudi tuendelee lakini nilivyorudi alikuwa ameshachukuliwa na Wasafi,” Majizzo ameeleza.

Kwa siku za hivi karibuni, mapokezi ya watangazaji kwenye vituo vya redio yamekuwa na ‘mbwembwe’ za aina yake. Wasafi FM/TV waliwapokea watangazaji kutoka E-FM kwa helicopter aka chopa.

Lakini Majizzo na timu yake wao wameweka mtandaoni kipande cha video kinachowaonesha wawakilishi wa E-FM/TV wakimtoa kifungoni Jonijoo.

Hata hivyo, Majizzo ameeleza kuwa hiyo ilikuwa sehemu ya vipande 37 vya tamthilia itakayorushwa ‘E-TV’.

“Hapana, mimi kama mfanyabiashara kila kitu ni fursa… kwahiyo, hiyo ni ‘series’ ya TV ambayo ina episodes nyingi tu, hata kesho nita-post episode nyingine, kuna episodes kama 37 hivi,” ameeleza Majizzo.

Ingawa Majizzo amesawazisha mlima wa vitendawili hivyo, bado kuna kitendawili kingine kinachoendelea mtandaoni, ambapo wengi wanasadiki kuwa Jonijoo ameondoka Wasafi FM baada ya Lil Ommy kusajiliwa na kituo hicho.

Lil Ommy ambaye awali alikuwa akifanya kazi na Jonijoo Times FM, alisajiliwa Wasafi FM na kuanzisha kipindi kipya kilichopewa jina la ‘The Switch’, kipindi ambacho kimeonekana kuwa na maudhui yaliyokuwa yanafanana na yale ya kipindi cha Block 89 kilichokuwa cha Jonijo.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro apata maambukizi ya corona, azungumza

Corona: Hospitali ya Nairobi kupima sampuli 900 kwa siku, kupima ni Sh 200,000

Tetesi za usajili barani Ulaya
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro apata maambukizi ya corona, azungumza