Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, amesema wakati umefika wa kuwa na watumishi wenye weledi wa kutosha kwenye Halmashauri zote nchini na pia hazitakiwi kuwa pango la wezi, wazembe au jalala la kutupa wabadhilifu walioshindikana kwingineko.

Aidha, Waziri Mkuu amesemma Serikali za Mitaa na Halmashauri zote nchini zinatakiwa zianze kujitathmini na kujipanga vizuri zaidi kuona ni kwa namna gani zitakuwa chachu ya maendeleo ya viwanda vinavyotarajiwa.

Ameyasema hayo mapema hii leo wakati akifungua Kikao cha Baraza la Mashauriano (RCC) mkoani Dodoma. amesema kikao ni chombo muhimu na endapo kitatumika vizuri kitaweza kusaidia kusukuma maendeleo ya Mkoa na kupunguza migogoro kwenye Halmashauri.

Aidha, Majaliwa amesema Serikali itaendelea kuongeza kiwango cha ruzuku kwa Halmashauri zote nchini kwa kadiri uwezo utakavyoruhusu na kusisitiza kwamba fedha hizo lazima zisimamiwe vizuri na zielekezwe kwenye miradi ya maendeleo inayowagusa wananchi.

“Endapo itabainika kwamba kuna baadhi ya Sheria zinazokwamisha utendaji katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, hatutasita kuzifanyia mapitio na hatimaye kuzibadili ili ziendane na azma yetu ya kutoa huduma bora kwa wananchi,” amesema Majaliwa.

 

Hata hivyo Waziri Mkuu amesema vyanzo vingi vya mapato ya Serikali vinapatikana kwenye Halmashauri huku changamoto kubwa ikiwa ni kulegalega kwa  Halmashauri nyingi katika ukusanyaji wa mapato ya kodi na yasiyo ya kodi jambo linalozorotesha utoaji wa huduma kwa wananchi.

 

Video: TFF yazindua programu maalumu ya kushiriki olympic
Mpogolo: Vijana fanyeni mazoezi kuepuka maradhi