Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu jijini Dar es Salaam, leo imeridhia ruhusa ya Mbunge wa Kawe, Halima Mdee kuendelea na shughuli za kibunge nchini Burundi baada ya kushindwa kufika mahakamani kusikiliza kesi inayomkabili.

Uamuzi huo umefikiwa baada ya mdhamini wa Mdee kuwasilisha Mahakamani hapo nakala ya barua ya Katibu wa Bunge ya kumuombea ruhusa mbunge huyo ili akashiriki michezo na timu ya Bunge nchini Burundi. Hakimu alikubaliana na barua hiyo akieleza kuwa iliwasilishwa pia ofisini kwake.

Kwa upande wa Serikali, Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi aliiambia mahakama hiyo kuwa hana pingamizi lolote kutokana na barua iliyowasilishwa, kuhusu ruhusa ya Mdee.

Hakimu aliahirisha kesi hiyo na kumtaka Mdee kuhakikisha anahudhuria kesi hiyo Desemba 21 mwaka huu, amri ambayo ilitolewa pia kwa mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche ambaye alitakiwa kufika mahakamani hapo lakini alikuwa na ruhusa ya kumuuguza mkewe.

Mdee, Heche, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko, Katibu Mkuu wa chama hicho, Dkt. Vincent Mashinji na wengine wanakabiliwa na mashtaka 13 ikiwa ni pamoja na uchochezi, kuchochea uasi na kuwahamasisha wafuasi wao kufanya makosa na kufanya maandamano yasiyo na kibali Februari 16 mwaka huu.

‘Wajanja’ wapiga asilimia 60 ya umeme wa Serikali
Serikali yaagiza kusajiliwa kwa mafundi simu