Siku moja baada ya kuanza mazoezi kujiandaa na mwendelezo wa mechi za Ligi Kuu ya Tanzania Bara, pamoja na michuano ya Kombe la FA na Mapinduzi, kocha mkuu wa Yanga George Lwandamina amefuraishwa na urejeo wa kiungo Mkongoman Papy Kabamba Tshishimbi.

Katika mahojiano na mtandao wa GOAL, Lwandamina amesema Tshishimbi ni mchezaji muhimu ndani ya kikosi chake na kukosekana kwake mechi mbili kumewalazimu kupambana sana hata kupata ushindi.

“Wachezaji wanaocheza kwenye eneo hilo siyo wabaya lakini tatizo ni uzoefu wao mdogo, ukilinganisha na Shishimbi, kwaiyo kupona kwake na kurejea dimbani kutakuwa na faida kwa Yanga, kutokana na mikakati tuliyokuwa nayo kuhakikisha tunamaliza ligi tukiwa mabingwa,”amesema Lwandamina.

Kocha huyo raia wa Zambia amesema anachosubiria kwasasa ni kurejea kwa wachezaji wengine watatu kiungo Thabani Kamusoko, Amissi Tambwe na Donald Ngoma ambao wapo nje wakikabiliwa na majeruhi ya muda mrefu sasa.

Lwandamina amesema kama wachezaji hao wote wakamaliza matatizo yao ya nje ya uwanja na kuwafiti haoni timu ambayo inaweza kuwazuia kutetea ubingwa wao ambao wanaushikilia kwa mara ya tatu mfululizo.

Papy Kabamba Tshishimbi amekosa mechi mbili za Yanga kutokana na kuumia misuli ya paja ambayo ilimweka nje na kumweka katika wakati mgumu na nafasi yake kuchukuliwa na Patto Ngonyani ambaye kiwango chake kimewavutia wengi.

Makala: Mudathir Yahya anapotupa maana ya mchezaji wa mkopo
Wadau wa soka kuendesha majaribio kwa wachezaji wa jinsia zote