Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amesema hakubali kuikimbia nchi yake hata kama jeshi la polisi halijamhakikishia usalama wake ameahidi kurejea nyumbani muda wowote kutoka sasa, mara baada ya kushauriana na madaktari wake.

“Pamoja na kwamba, waliotaka kuniua mchana kweupe katikati ya mji wa Dodoma, bado wanaitwa watu wasiojulikana; pamoja na kwamba sijahakikishiwa usalama wangu na vyombo vya usalama vya serikali ya John Magufuli, bado sitakubali kuishi uhamishoni.” Amesema Lissu.

Lissu amesema hayo jana akifanya mazungumzo na waandishi wa habari na kudai kuwa alikuwa akirejea kuwashukuru wananchi ndani na nje ya nchi, mashirika ya ndani na kimataifa, kwa msaada waliompa wakati wa matibabu yake.

Lissu alishambuliwa kwa risasi takribani 39 na watu wasiojulikana tarehe 7 Septemba 2017. Kwa mujibu wake, kati ya risasi hizo, risasi 16 ziliingia kwenye mwili wake.

Aidha amesema bado anafanya mashauriano ya tarehe kamili ya kuwasili nchini.

“kwa hiyo, wakati muafaka utakapofika, hopefully (nina matumaini) sio mbali sana, nitawaeleza tarehe kamili ya kurudi; na kwa mlioko Dar es Salaam, nitawaomba mniandalie supu ya utumbo wa mbuzi pale Rose Garden kwa Mzee Assey.”

Akizungumzia hali yake ya kiafya, Lissu amesema, kwa sasa majeraha yake yameanza kupona, hivyo anafanya mazoezi ya viungo pamoja na kusubiri kupimwa urefu wa mguu wa kulia.

Kanisa laanguka, 13 wapoteza maisha
Lissu akunja mamilioni ya posho, mishahara ya miezi mitatu