Mkurugenzi Mkuu wa Clouds Media Group, Joseph Kusaga ametangaza ratiba ya msiba wa aliyekuwa mtangazaji wa Clouds FM, Ephraim Kibonde uliotokea alfajiri ya leo jijini Mwanza.

Kusaga amesema kuwa mwili wa Marehemu Kibonde utawasili jijini Dar es salaam leo saa nne usiku katika Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ukitokea jijini Mwanza alipokuwa akipatiwa matibabu.

Amesema kuwa baada ya kuupokea mwili wa Ephraim Kibonde utapelekwa moja kwa moja hospitali ya Lugalo, ambapo shughuli za maombolezo zitaendelea nyumbani kwake Mbezi jijini Dar es salaam huku mazishi yakitarajiwa kufanyika siku ya jumamosi.

”Leo tarehe 7 mwezi wa tatu, Clouds Media imepata pigo jingine kubwa kwa kumpoteza mtangazaji wake mahiri, Ephraim Kibonde, saa moja nilipigiwa simu kujulishwa kuhusu kifo cha ndugu yetu, matatizo yalianza kumpata akiwa Bukoba kwenye msiba wa mkurugenzi mwenzangu, Ruge Mutahaba, tukampeleka hospitali ya Bukoba na baaye tukampeleka jijini Mwanza kwa matibabu zaidi, lakini huko ndiko umauti ulipomkuta,”amesema Kusaga

Kylie avunja rekodi ya ubilionea akiwa kinda, atumia mitandao ya kijamii
Siza wa Clouds FM asimulia kilichompata Kibonde kabla ya kupoteza maisha