Kaya zaidi ya 2086 za vitongoji viwili vya Migombani-Mbuyuni na Mchangani Kijiji cha Kirambo kata ya Tangazo Tarafa ya Kitaya mkoani wa Mtwara wamelazimika kuyahama makazi yao kwa kutumia Mitumbwi baada ya kuzingirwa na Maji kufuatia kufurika kwa Mto Ruvuma unaotenganisha eneo hilo na nchi jirani ya Msumbiji.

Katika eneo hilo kumeripotiwa kutokea kwa uharibifu wa zaidi ya Ekari 3014 za Mpunga na Mahindi na serikali imesha peleka Boti kwa ajili ya kutoa msaada kwa wananchi hao ili kuweza kuondoka katika maeneo hatalishi.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Maafa wa Kata ya Tangazo ambaye pia ni Diwani wa Kata hiyo, Ramadhani Said wakati akitoa taarifa kwa mkuu wa wilaya ya Mtwara, Evod Mmanda ambapo amesema kuwa maeneo yaliyoathirika ni Vitongoji viwili vilivyopo pembezoni mwa Mto Ruvuma ambavyo vimekubwa na mafuriko hayo baada ya Mto kuzidiwa.

“Katika vijiji hivi viwili tuna jumla ya waathirika 2086 ambapo Kitongoji cha Migomba-Mbuyuni kuna kaya 306 na kitongoji kingine cha Mchangani kuna kaya 326 zilizoathirika ambapo katika kaya hizo kuna idadi kubwa ya watu wakiwemo wanafunzi wa shule za Msingi,”amesema Diwani huyo

Wakizungumzia hali hiyo, baadhi ya wananchi walioathirika akiwemo, Fatuma Selemani pamoja na Khadija Salum wamesema kuwa hali hiyo imekua ikijitokeza mara kwa mara ambapo wameiomba serikali kuwa karibu nao hususani katika kipindi hiki wakidai jambo hilo limekuja kwa dharula na wengi wao wamekutwa wakiwa mashambani na hali inavyoelekea huenda wakakabiliwa na balaa la Njaa.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Mtwara, Evod Mmanda akizungumza na wananchi walioathirika amesema tayari amefanya jitihada za haraka na kufanikisha kupata Boti ya kuwavusha wananchi pamoja na baadhi ya mizigo ambayo bado haijaharibika akisisitiza viongozi wa kamati ya maafa ya kata kuweka utaratibu wa kutumia Boti hiyo kwa kuweka kipaumbele kwa makundi maalum wakiwemo Wazee, na watoto.

Hata hivyo kwa mujibu wa kamati ya Maafa ya kata tayari wameandaa utaratibu ambapo wananchi wote walio athirika watasafirishwa na kwenda kuishi kwa ndugu zao katika vijiji jirani kwani sehemu kubwa ya wakazi hao wametoka katika vijiji vilivyo jirani na hakuna wageni ambao watakosa mahali pa kuishi.

Tanesco Songwe wapewa siku tatu kujieleza
Video: Chadema tutaingia mtaani mchana kweupe, Kansa yamtesa Baba wa Diamond