Shirikisho la soka nchini Hispania limetangaza adhabu ya kumfungia michezo miwili mshambuliaji wa FC Barcelona Ousmane Dembele, kufuatia kadi nyekundu aliyoonyeshwa wakati wa mchezo wa La Liga dhidi ya Sevilla mwishoni mwa juma lililopita.

Dembele alionyeshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja na mwamuzi Antonio Mateu Lahoz, baada ya kutokea majibishano baina ya wawili hao, kufuatia maamuzi yaliyochukuliwa dhidi ya FC Barcelona.

Dembele alikumbwa na adhabu hiyo dakika chache baada ya kuifungia FC Barcelona bao la pili, ambalo ni miongoni mwa mabao manne yaliyoipa ushindi klabu hiyo ya Camp Nou dhidi ya Sevilla.

Taarifa ya shirikisho la soka nchini Hispania imeeleza kuwa, mshambuliaji huyo kutoka nchini Ufaransa, alimtolea lugha chafu mwamuzi Antonio Mateu Lahoz, baada ya kujiridhisha kupitia ripoti iliyowashilishwa mara baada ya mchezo huyo.

Kwa maamuzi hayo, Dembele atakosa mchezo wa dhidi ya Real Madrid ‘El Clasico’, ambao utatanguliwa na ule dhidi ya Eiber, utakaochezwa mwishoni mwa juma lijalo.

FC Barcelona watakuwa wenyeji wa Real Madrid katika mchezo wa La Liga, uliopangwa kuchezwa Oktoba 26.

Wakati huo huo beki Gerard Pique ataendelea na adhabu ya kukosa mchezo mmoja dhidi ya Eibar, kufuatia kuonyeshwa kadi ya njano wakati wa mchezo dhidi ya Sevilla.

Pique alifikisha idadi ya kadi tano za njano, ambazo kisheria zinamtaka kukosa mchezo ujao, na tayari ilihisiwa alifanya kosa la kuupiga mpira kwa makusudi uliokua umeshatoka, ili aonyeshwe kadi.

Shirikisho la soka nchini Hispania limethibitisha hakuna ushahidi wa halali kama beki huyo mwenye umri wa miaka 32 alifanya kitendo hicho kwa makusudi ama la.

NEC: Kadi ya mpiga kura haitatumika kwenye uchaguzi serikali za mitaa
Video: Tamu ya ujenzi Barabara Tandale yageuka Chungu, Watoto wazama shimoni, Osha waingilia kati