Kamati ya nidhamu ya Shirikisho La Soka Nchini TFF imewafungia Bernard Morrison (Young Africans) na Jonas Mkude (Simba SC) kila mmoja mechi mbili pamoja na faini ya shilingi lakini tano (500,000) kutokana na vitendo ambavyo si vya kiungwana. Adhabu hiyo inaanza mara moja kuanzia leo Jumatano.

Morrison amekumbana na adhabu hiyo baada ya kumpiga kiwiko mchezaji wa Tanzania Prisons wakati Jonas Mkude yeye alifanya hivyo kwa mchezaji wa Biashara United.

Hata hivyo wawili hao huenda ikawa ahuweni kwao kutumikia adhabu ya kukosa michezo miwili ya Ligi Kuu Tanzania Bara, zaidi ya kuumizwa na kiasi cha fedha ambacho wametozwa kama faini.

Mkude amekua nje ya kikosi cha Simba SC tangu Ligi iliporejea Juni 13, kufuatia majeraha ya mguu yanayomsumbua, huku Morrison akiingia kwenye mzozo na uongozi wa klabu ya Young Africans, na huenda akawa na nafasi finyu ya kucheza kwa siku za karibuni.

Kiungo huyo kutoka Ghana ameibua sakata la kutoutambua mkataba wa miaka miwili ambao unadaiwa aliusaini, kufuatia kiwango chake kuwaridhishwa viongozi wa Young Africans mara baada ya kusajiliwa wakati wa dirisha dogo la usajili.

Mbali na Morrison kutozwa faini ya shilingi 500,000 na TFF, pia kiungo huyo aliegeuka kipenzi cha mashabiki wa Young Africans, ameadhibiwa kwa kutozwa faini ya shilingi milioni moja na nusu (1500,000) na uongozi wa klabu, kwa kosa la kuzungumza na vyombo vya habari bila ruhusa maalum.

Urais 2020: Mwanamichezo achukua fomu Zanzibar
Mwanamke wa pili ajitosa urais Zanzibar