Mahakama ya Hakimu mkazi Kisutu imemuachia huru mwandishi wa Habari za Uchunguzi Erick Kabendera, huku ikimtaka kulipa faini kwa makosa yake yote mawili ikiwemo utakatishaji fedha na kukwepa kulipa kodi, hii ni baada ya kuondolewa shtaka la Kuongoza genge la Uhalifu.

Katika hukumu iliyosomwa na Hakimu Janeth Mtega imemtaka mtuhumiwa Erick Kabendera kulipa kiasi cha pesa za kitanzania shilingi laki mbili na elfu Hamsini (250,000) au kutumikia kifungo cha Miezi mitatu jela. Adhabu hiyo inaambatanana fidia ya Shilingi za kitanzania Milioni 172, hii ni kwa kosa la kushindwa kulipa kodi.

Kosa la pili limemtaka Erick Kabendera kulipa faini ya shilingi za kitanzania Milioni mia Moja (Mil 100) hii ikiwa ni adhabu kwa kosa la Utakatishaji fedha katika kesi ya Uhujumu uchumi inayomkabili.

Julai 29, 2019 kuliibuka utata baada ya Kabendera kudaiwa kuchukuliwa na Watu wasiojulikana nyumbani kwake Mbweni-Dar lakini Julai 30 Polisi ilithibitisha kumkamata Mwandishi huyo na kusema hajatekwa.

Julai 31, 2019 Idara ya Uhamiaji Nchini ilithibitisha kumshikilia Kabendera huku kwa kusema kuwa ilikuwa na shaka na uraia wake jambo lililopingwa na Marehemu mama yake mnamo Agosti 3, 2019.

Agosti 5, 2019 Kabendera alifikishwa kwa mara ya kwanza Mahakamani na kusomewa mashtaka matatu, Kujihusisha na Mtandao wa Uhalifu, Kukwepa Kodi ya zaidi ya Tsh. Milioni 173.2 na Kutakatisha fedha.

Mbeya: Madiwani 11 wa Chadema wajiunga CCM
NIDA washusha mitambo kufyatua vitambulisho 9,000 kwa saa