Beki John Stones amekosa nafasi ya kucheza dhidi ya klabu yake ya zamani ya Everton katika mchezo wa ligi kuu ya soka nchini England wa mwishoni mwa juma hili, kufuatia majeraha ya kichwa yanayomkabili.

Manchester City watapambana na Everton kwenye uwanja wa Goodison Park kesho jumamosi, huku wakiwa na lengo la kuendelea na mikakati ya kusaka ushindi ambao utawasogeza katika mafanikio ya kutwaa ubingwa msimu huu.

Meneja Pep Guardiola amesema leo ijumaa kuwa, Stones hatoweza kucheza mchezo huo utakaoanza mishale ya saa moja na nusu kwa saa za Afrika Mashariki, kutokana na majeraha ya kichwa aliyoyapata akiwa katika timu ya taifa.

Stones aliumia wakati wa mchezo wa kimataifa wa kirafikid dhidi ya Italia, uliomalizika kwa timu hizo kwenda sare ya kufungana bao moja kwa moja katika uwanja wa Wembley siku ya jumanne.

“Anaendelea vizuri lakini hatoweza kucheza mchezo wa kesho, anahitaji kupumzika ili apate muda wa kupona vizuri kwa ajili ya michezo mingine itakayotukabili siku za usoni,”

“Mashabiki wengi walimtarajia katika mchezo wa kesho, kwa sababu angepata kucheza ilikua ni heshima kubwa kwake kutokana na uhusiano uliopo kati yake na mashabiki wa Everton, lakini hatuna budi kumpumzisha.” Amesema Guardiola.

Stones aliondoka Everton baada ya kusajiliwa na Man City mwaka 2016 kwa ada ya uhamisho ya Pauni milioni 47.5 sawa na dola za kimarekani milioni 67.

Katika hatua nyingine Guardiola amesema mshambuliaji Sergio Aguero, ambaye alikosa michezo miwili ya kimataifa ya kirafiki dhidi ya Italia na Hispania kufuatia majeraha ya goti, yupo katika hati hati za kuukosa mchezo wa kesho dhidi ya Everton.

Wilder agoma kuhudhuria pambano la Joshua na Parker kisa ‘ubabe’
Liverpool kuivaa Crystal Palace bila Joe Gomez, Emre Can