Maafande wa JKT Ruvu wameanza safari ya kuelekea mkoani Kagera, tayari kwa mchezo wa ligi kuu ya soka Tanzania bara ambao umepangwa kuunguruma mwishoni mwa juma hili kwenye uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.

JKT Ruvu wameondoka mkoani Shinyanga walipokua wanakabiliwa na mchezo wa ligi kuu mwishoni mwa juma lililopita, ambapo walipambana na Mwadui FC na kuambulia sare ya mabao mawili kwa mawaili.

Afisa habari wa klabu hiyo inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa, Constantine Massanja amesema wameanza safari ya kuelekea mkoani Kagera, huku wachezaji wao wakiwa katika hali nzuri na wanaamini watafanikisha mpango wa kupambana na kupata ushindi kwenye uwanja wa Kaitaba.

“Tumeondoka mkoani Shinyanga, morari ya wachezaji ipo juu baada ya kuona matunda ya kujiandaa vyema kwa majuma matatu ambapo ligi kuu ilikua imesimama, kwa hakika ilikua bahati mbaya sana kwetu kulazimishwa matokeo ya sare na Mwadui FC kwa sababu tuliweza kuwamudu na kuwatangulia mabao mawili kwa moja, lakini dakika za lala salama mchezaji wetu aliuna mpira eneo la hatari na tukaadhibiwa kwa penati,” alisema Massanja. 

“Tunaamini mapungufu yaliyojitokeza katika mchezo wetu na Mwadui FC yatafanyiwa kazi na kaimu kocha mkuu King Abdallah Kibadeni ambaye ameachiwa jukumu hilo na kocha Bakari Shime, ambaye kwa sasa yupo katika majukumu ya kukinoa kikosi cha Serengeti Boys,” aliongeza.

Kuhusu vita ya kuwania kusalia kwenye ligi kuu msimu wa 2017/18, Massanja amesema wataendelea kupambana ili kutimiza lengo hilo japo amekiri lina changamoto zake, kutokana na mwenendo wa ligi.

“Hatutaki kupiga hesabu za point tunazotakiwa kuzipata katika michezo mitano iliyosalia, lolote linaweza kujitokeza kwa mujibu wa kanuni za ligi, tunaweza kufanya makosa kama binaadamu na tukaadhibiwa, kwa mfano kosa la kumchezesha mchezo ambaye anaweza kutokua na sifa za kucheza kwa kuwa na kadi tatu za njano, na mwishowe tukajikuta tunaadhibiwa na bodi ya ligi, hivyo hatutaki kujihusha na hesabu hizo, lililo mbele yetu ni kupambana kisawa sawa,

“Kila timu kwa sasa ipo katika hali ya kupambana na kwa kulitambua hilo hatuna budi kufanikisha mipango ya kukataa kupoteza point tatu za mchezo wowote unaotukabili kuanza sasa.” Amesema Massanja.

Ruvu JKT inatakiwa kushinda michezo yote iliyosalia ili kujihakikishia nafasi ya kucheza ligi kuu msimu ujao, kinyume na hapo itakua kwenye hatari ya kuwa miongoni mwa timu tatu zitakazoshuka daraja mwishoni mwa msimu huu.

Kwa sasa, JKT Ruvu inaburuza mkia kwa kuwa na point 22 wakitanguliwa na Majimaji FC wenye point 23, Toto Africans wenye Point 23, Mbao FC wenye point 27, Ndanda FC na Stand Utd wenye point 28 kila mmoja.

Serikali kuchukua hatua zaidi dhidi ya ndoa za utotoni
Video: Prof. Mkumbo ateuliwa kuwa Katibu Mkuu Wizara Maji