Mtuhumiwa wa vitendo vya ujambazi ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Nyarero Wilayani Tarime mkoani Mara, Bahati Nyakiha ameuawa huku wenzake watatu wakikimbia kusikojulikana wakati wakijihami kwa kuwafyatulia risasi askari Polisi ambapo pia Polisi wamefanikiwa kukamata Bunduki aina ya SMG ikiwa na risasi 4 waliokuwa wakiitumia kufanya majibishano.
 
Hayo yamesemwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Polisi Tarime /Rorya, Henry Mwaibambe ambapo amesema kuwa Mei 2, 2019 majira ya Saa 9 usiku katika Kijiji cha Nkerege Kata ya Kiore Askari Polisi wakiwa wanafuatilia nyendo za wahalifu waliokuwa wanataka kufanya uporaji katika moja ya duka la vifaa vya ujenzi mjini Tarime ambalo hakulitaja jina wala mmiliki wake, na baada ya watuhumiwa hao kuwaona Polisi wanawafuatilia walianza kujihami kwa kuwafyatulia Risasi Polisi huku wakiwa wanakimbia.
 
Amesema kuwa Polisi nao waliwajibu na kufanikisha kumpiga risasi jambazi mmoja, Bahati Nyakiha maeneo ya mgongoni na kuanguka chini ambapo majambazi hao walifyatua risasi nne kuelekea upande waliokuwa Askari Polisi.
 
“Jambazi huyo alikimbizwa Hospitali ya wilaya ya Tarime kwa matibabu na alifariki muda mfupi baada ya kufikishwa hospitalini na mwili wake umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti na kwamba ndugu jamaa wa marehemu wameombwa kwenda kuutambua mwili huo,”amesema Kamanda Mwaibambe
 
Aidha, ameongeza kuwa Mtuhumiwa huyo kwa muda mrefu amekuwa akifuatiliwa kutokana na kujihusisha na vitendo vya uhalifu na kwamba watuhumiwa wengine bado wanatafutwa.
 
Kwa upande wake Chacha Marwa mkazi Nyarero amesema kuwa mtuhumiwa aliyeuwawa alikuwa akituhumiwa na wananchi kwa wizi ikiwemo wizi wa Ng’ombe na amekuwa akiiba Mali za wananchi maeneo mbalimbali na kwamba tukio hilo liwe fundisho kwa watu wote wanaojihusisha na ujambazi huku akilipongeza Jeshi la Polisi kwa juhudi za kupambana na wahalifu.

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Mei 5, 2019
RC Mwangela atoa agizo kuhusu Dampo