Msanii wa maigizo ya filamu nchini, Irene Uwoya amewaomba radhi waandishi wa habari kufuatia kitendo alichokifanya jana wakati wa mkutano na waandishi wa habari baada ya kuwamwagia pesa na kujikuta wakiachilia camera zao na kuanza kudaka fedha hizo hali iliyopelekea baadhi ya waandishi kuharibu baadhi ya vifaa vyao kutokana na vurugu zilizotokea wakati wa kudaka fedha hizo.

Irene amesema hakufanya hivyo kwa lengo la kudhalilisha waandishi wa habari kama ambavyo imetafsiriwa na watu wengi, kwani dhahiri anatambua umuhimu mkubwa wa waandishi wa habari katika jamii.

”Kama binadamu moyo wangu ulijawa na upendo na furaha iliyopitiliza ndipo niliona niweze kushiriki nanyi furaha hiyo kwa aina ile ya kuwatunza pesa, sababu mara nyingi mmekuwa watu muhimu katika kazi na mambo yote yanayohusu sanaa yetu na jamii kwa ujumla…,na baadhi ya waandishi ambao kwa bahati mbaya waliharibu vifaa vyao wakati wa kuokota shukrani yangu (pesa) naomba mniwie radhi na mnisamehe sana na poleni sana kwa changamoto”. amesema Uwoya.

Aidha, tukio hilo limetafsiriwa tofauti na baadhi ya watu na kusema kuwa kitendo hiko ni kuwadhalilisha waandishi wa habari na kuwafanya waonekane na njaa.

Baadhi ya watu maarufu katika mitandao ya kijamii wamemjia juu msanii huyo kwa kitendo hiko na kusema kuwa upo utaratibu mzuri unaofahamika na kutumiwa na watu katika utoaji pesa kwa waandishi wa habari kama nauli yao mara baada ya kumaliza kufanya nao kazi, ambayo imezoeleka ni ile ya kuweka hela kwenye bahasha na kuwakabidhi na si kutoa hela kwa kuzirusha kama ambavyo amefanya Irene Uwoya siku ya jana.

Kupitia ukurasa wa Instagram Uwoya ameandika waraka mrefu wa kuwaomba radhi wanadishi wa habari pamoja na watu wote waliokwazika na kitendo huko.

Hayo yametokea jana wakati wa mkutano wa wasanii wa filamu za bongo na waandishi wa habari katika uzinduzi wa mtandao wa Swahili inflix ambao utawafanya watanzania kupakua filamu za kibongo na kuachana na ule utamaduni wa kununua CD kama ambavyo imekuwa siku za hapo nyuma.

Video: Ninyi ni sawa na majeshi mengine, msiichukie kazi yenu- JPM
Balozi Seif Idd atembelea eneo zitakapojengwa ofisi za SMZ