Mshambuliaji kutoka nchini Sweden Zlatan Ibrahimovic, amefunguka baada ya kuwa sehemu ya kikosi cha AC Milan kilichowabamiza mabingwa watetezi Ligi Kuu ya Italia Juventus FC mabao manne kwa mawili juzi Jumanne (Julai 07).

Juventus FC walikubali kipondo hicho ugenini mjini Milan, wakiongozwa na mshambuliaji wao mashuhuri duniani Cristiano Ronaldo raia wa Ureno.

Ibrahimovic amesema anaamini ubora wa kikosi cha AC Milan tangu aliposajiliwa klabuni hapo wakati wa dirisha dogo umeongezeka, na kama angetua San Siro mwanzoni mwa msimu huu klabu hiyo, ingetwaa ubingwa wa Ligi Kuu Italia ‘Serie A’.

AC Milan ipo nafasi ya saba kwenye msimamo wa Ligi Kuu Italia ‘Serie A’ ikiwa na alama 49, huku Juventus FC wakiwa kileleni kwa kufikisha alama 75.

Mshambuliaji huyo mwenye miaka 38, ameonekana bado kuwa na makali  katika michezo mikubwa baada ya kufunga na kutoa assisti wakati AC Milan ikiizamisha Juventus FC kwenye uwanja wa San Siro juzi Jumanne.

Ibrahimovic ambaye amewahi kuzitumikia klabu kubwa duniani kama FC Barcelona, Ajax Amsterdam, Inter Milan na Manchester United amesema kuwa iwapo angejiunga mapema na AC Milan timu hiyo ingeweza kutwaa taji la Ligi Kuu Italia ‘Scudetto’ “Kama ningekuwa hapa tangu mwanzo wa msimu nadhani ningeshinda Scudetto”.

“Kuna mambo yapo tu, huwezi kuzuia. Ibrahimovic  ni mfano mzuri kwa vijana wa  Milan ambao ni wachezaji wenzake. Mimi ni rais, kocha na mchezaji, lakini wananilipa kama mchezaji,” alisema Ibrahimovic.

Mshambuliaji huyo na nahodha wa zamani wa timu ya taifa la Sweden mkataba wake na AC Milan unatarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu licha ya mchango wake katika kikosi hicho, haijafahamika kama ataendelea kusalia AC Milan au la.

Sababu za hatma ya Zlatan ndani ya AC Milan kutoamriwa mapema zimetajwa ni kusubiria mipango ya kocha mpya Ralf Rangnick ambaye atainoa timu hiyo msimu ujao kuchukua nafasi ya Stefano Pioli.

Salamu za pongezi zamiminika Simba SC
Simba SC wabanwa Ruangwa, wakabidhiwa taji