Gari aina ya Passo lenye thamani ya Shilingi Milioni 8 za kitanzania lililoandaliwa kama zawadi kwa mrembo atakayeshinda shindano la Miss Lake Zone limekataliwa na waandaaji wa shindano la Miss Tanzania, The Look Company kwa kile walichosema kuwa haliendani na hadhi ya mashindano hayo.

Hata hivyo tayari waandaaji wa shindano la Miss Lake Zone wameandikiwa barua inayowataka kutafuta zawadi nyingine bora zaidi na barua hiyo tayari imetumwa Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA).

”Zawadi hiyo haiendani na hadhi ya mashindano najua wanajitahidi kutoa zawadi kubwa lakini kusema ukweli hatujaafiki” amesema Basilla Mwanukuzi ambaye ni Mkurugenzi wa The Look Company.

Aidha amesema waandaaji wa chini wa shindano hilo hawana ulazima wa kutoa zawadi kubwa bali kuwatafuta wasichana wenye vigezo na kuendesha shindano hilo kwa uweledi.

”Zawadi kubwa za magari inabidi watuachie sisi huku juu siyo kulazimisha, ninajua wana nia njema lakini hili hatukubaliani nalo” ameongezea Basilla.

Hata hivyo Fred Kikoti ambaye ni mwandaaji wa shindano la Miss Lake Zone amesema hana taarifa yeyote ya kukataliwa kwa zawadi hiyo.

Shindano la kumsaka Miss Lake Zone linatarajiwa kufanyika siku ya Kesho Agosti 4, 2018  jijini Mwanza ambapo warembo 15 watachuana vikali kutafuta zawadi ambayo hadi sasa haijafahamika rasmi mara baada ya The Look kuitolea nje zawadi iliyoandaliwa hapo awali.

Dondoo 10 za kukuwezesha kuhimili mazingira magumu ya kazi
Makocha wa timu za vijana Argentina wamrithi Sampaoli