Kamanda wa Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa, amesema mfanyabiashara Mohammed Dewji maarufu kama Mo, aliyepatikana leo baada ya kutekwa Oktoba 11, 2018, amesema watu waliomteka walikuwa wanataka fedha.

Akiongea leo nyumbani kwa baba yake Mo ambako alifika kumuona mfanyabiashara huyo, amesema amemweleza kuwa moja ya sababu ya kutekwa kwake ni fedha ambapo watekaji walikuwa wanataka wapewe fedha.

”Mo ameniambia tangu alipotekwa alikuwa amefungwa mikono, miguu na kufunikwa macho, lakini pia walimsimamia sana kwenye suala la kula lakini sababu kubwa watekaji walikuwa wanataka fedha ila walikuwa na hofu ya kumpigia baba yake wakiamini jeshi la polisi litawafikia”, amesema Mambosasa.

Mambo sasa ameongeza kuwa baada ya taarifa za jana kutoka kwa IGP Sirro kubaini gari lililotumika kumteka, zimesaidia kumpata mfanyabiashara huyo kwani wahusika waligundua wamekaribia kunaswa.

Kamanda Mambosasa pia amethibitisha kuwa gari lenye namba za usajili T 314 AXX, ambalo walilibaini kutumika kumteka Mo, likiwa na namba za nchi jirani AGX 404 MC, ndio hilo limetumika kumtelekeza katika eneo la Gymkhana jijini Dar es salaam.

Amemaliza kwa kusema baada ya kutupwa pale Gymkhana, walinzi wa eneo hilo walimuona na kumtambua kama ni Mo, ndipo wakamfungua kamba alizokuwa amefungwa kisha akawatajia namba za simu za baba yake na walipompigia mzee Dewji akafika na familia kumchukua.

Msako wawatia mbaroni raia wawili wa kigeni Dar
Kupatikana kwa 'Mo Dewji' viongozi mbalimbali wafunguka