Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoani Mbeya leo inatarajia kusoma hukumu ya kesi ya Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ na Katibu wa Chadema Kanda ya Nyassa, Emmanuel Masonga.

Washtakiwa hao wanadaiwa kutenda kosa la kutumia lugha ya fedheha dhidi ya Rais Dkt. Magufuli wakiwa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika mnamo Disemba 30, 2017 eneo la uwanja wa shule ya msingi Mwenge mjini Mbeya.

Jamhuri iliwasilisha mashahidi watano na kielelezo kimoja cha sauti iliyodaiwa kunaswa, sauti yenye maneno yaliyotolewa katika mkutano huo yenye zaidi ya dakika 39 na kuwasilishwa mbele ya Mahakama na Ispekta Joram Magova ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Tehama katika Ofisi ya Upelelezi Mkoani humo.

Aidha, kwa upande wa utetezi waliwasilisha mashahidi sita wakiwemo watuhumiwa wenyewe wawili waliokana kutamka maneno ambayo wanadaiwa kuyatoa kinywani mwao.

Hata hivyo, kwa mara ya kwanza, washtakiwa hao Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi “Sugu” na Katibu wa CHADEMA Kanda ya Nyasa, Emmanuel Masonga walifikishwa Mahakamani Januari 16 na kusomewa mashtaka na Wakili Mkuu wa Serikali, Joseph Pande ambapo kesi yao ilikuwa ikosomwa kwa muendelezo mpaka ilipofikia Februari 09, 2018 ambapo waliachiwa kwa dhamana ya milioni tano kwa kila mmoja.

 

Raia kupewa pesa zilizobaki bajeti ya 2017
Wimbi la utekaji nchini Uganda lawashtua wananchi