Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) limefungua kesi kwenye Kamati ya Nidhamu ya FIFA dhidi ya klabu ya Etoile Sportive du Saleh ya Tunisa kutokana na klabu hiyo kushindwa kuilipa klabu ya Simba SC ya Tanzania pesa za mauzo ya mchezaji Emmanuel Okwi.

Kwa mujibu wa barua ya FIFA kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Tunisia (FTF) na nakala yake kwenda TFF, klabu hiyo inashitakiwa  kwa kuvunja kanuni kwa mujibu wa ibara ya 64 ya kanuni za nidhamu za FIFA (Fifa Disciplinary Code).

Kwa kuzingatia hilo, agenda hii itakuwa kwenye kikao kijacho cha kamati ya nidhamu.

Etoile Sportive du Sahel wametakiwa kulipa mara moja kiasi cha dola za kimarekani laki 3 na riba ya asilimia 2% kwa kila mwaka kama ilivyoelekezwa na maamuzi ya Jaji mmoja wa Kamati ya Nidhamu za Wachezaji mnamo tarehe 20 Novemba 2014.

Tangu wakati huo Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limekua likiwasiliana na Shirikisho la Mpira wa Miguu la Tunisia (FTF) na FIFA kwa niaba ya klabu ya Simba amabye ni mwanachama wa TFF.

Ikiwa klabu hiyo ya Tunisia itafanya malipo kwa klabu ya Simba na kupelekea ushahidi wa malipo kwa FIFA basi suala hilo litafutwa.

Aidha klabu hiyo iko kwenye hatari ya kushushwa daraja au kupokwa alama  kwenye ligi (League Point) iwapo haitalishughulikia suala hilo mara moja.

Malinzi Afunga Fainali Za Airtel Rising Stars 2015
Orodha Ya Wanamichezo Matajiri Duniani