Familia ya bilionea Mohammed Dewji, imesimulia namna ambavyo kijana wao alivyoachiwa na watekaji usiku wa kuamkia leo.

Msemaji wa familia hiyo, Azziz Dewji ameviambia vyombo vya habari kuwa watekaji hao walimuachia huru bilionea huyo kijana majira ya saa 8 usiku, Oktoba 20.

Alieleza kuwa baada ya kumuachia, Mo Dewji alimpigia simu baba yake na kisha kurejea rasmi nyumbani kwao.

“Yuko hapa nyumbani tunamshukuru Mungu. Walimuachia majira ya saa nane na nusu usiku halafu yeye akapiga simu kwa baba yake,” alisema Azziz.

Aliongeza kuwa afya ya bilionea huyo ni nzuri kwa asilimia 100 na kwamba kama kuna tatizo litakuwa tatizo la kisaikolojia kutokana na kutekwa.

Aidha, alimshukuru Rais John Magufuli, vyombo vya usalama pamoja na wananchi kwa juhudi za kupatikana kwa mwanaye.

Mo alitekwa saa 11 alfajiri ya Oktoba 11 mwaka huu, katika hotel ya Colosseum iliyoko Oysterbay jijini Dar es Salaam, alipokwenda kufanya mazoezi.

Familia yake imesema kuwa itazungumza na vyombo vya habari leo kuhusu kupatikana kwa kijana wao ambapo naye atahudhuria mkutano huo.

DNA ya jasho la nguo yamshika mbakaji na muuaji wa watoto
Alichokiandika 'Mo Dewji' baada ya kupatikana akiwa hai