Wachezaji watano na baadhi ya wafanyakazi wa klabu ya Valencia ya Hispania, wamefanyiwa vipimo na kubainika wapo salama dhidi ya janga la ugonjwa wa Covid-19 unaosababishwa na virusi vya Corona, linaoendelea kuitesa dunia kwa sasa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na klabu hiyo, imeeleza kuwa utaratibu wa kuwafanyia vipimo wachezaji na wafanyakazi umekua ukiendelea klabuni hapo, baada ya beki kutoka Argentina Ezequiel Garay, kutangaza kuwa mchezaji wa kwanza katika ligi ya La Liga aliekutwa virusi vya Corona.

Mbali na Garay beki wa kati wa Valencia Eliaquim Mangala, naye amekiri kufanyiwa vipimo na kukutwa na virusi vya Corona, na baadae alitengwa kwa kusudio la kutowaambukiza wachezaji wengine.

“Ni wazi nimefanyiwa vipimo, na kwa bahati mbaya nimekutwa na maambukiza ya virusi vya Corona,” ameandika Garay mwenye umri wa miaka 33, kwenye ukurasa wake wa Instagram.

“Kwa kweli nipo vizuri na sijisikii maumivu ya aina yoyote, lakini ninaheshimu misingi ya kiafya, ili nifanikishe lengo la kuishi katika afya njema na kutowaambukiza wengine.”

Kwa upande wa beki wa zamani wa Manchester City ya England, Mangala ameandika: “Nimelifahamu hili leo (Jana Jumapili), lakini nimelipokea katika misingi ya kutambua nimeathirika na virusi vya Corona. Kiuhalisia nipo vizuri kimwili na sihisi maimivu yoyote, na bado sijaonyesha dalili zozote kama nimeathirika. Nilichokifanya ni kuthibitisha kuwa nimegundulika nina virusi vya Corona, nitaendelea kujitenga na watu wengine hadi hali yangu itakapokua salama.”

Nchi ya Hispania inaripotiwa kuwa nchi ya pili kuwa na wagonjwa wengi, ikitanguliwa na Italia katika bara zima la Ulaya.

Tayari ligi kuu ya soka ya nchi hiyo (La Liga) imesimamishwa, huku klabu ya Real Madrid ikiripotiwa kufanya maamuzi yakuwaweka Karantini wachezaji wake wote.

Hatma ya UEFA Champions League, Europa League kujulikana kesho
Video: Halima Mdee, Esther Bulaya kupandishwa tena kizimbani, Corona yasitisha sherehe za pasaka