Rapa na mtayarishaji wa muziki, Diddy ameripotiwa kuachana na mpenzi wake wa muda mrefu, mwimbaji Cassie Ventura.

Kwa mujibu wa vyanzo vya karibu vilivyokaririwa na jarida la People, wawili hao waliachana miezi kadhaa iliyopita lakini waliamua kubaki kama marafiki.

“Uamuzi wao ulitokana na makubaliano kati yao na wamebaki kuwa marafiki tu. Cassie amesema atajikita zaidi kwenye muziki wake na uigizaji,” chanzo kimeliambia jarida la People.

Cassie alisainiwa na lebo ya Bad Boy Records inayomilikiwa na Diddy mwanzoni mwa miaka ya 2000. Mwaka 2007, tetesi za kuwa na uhusiano wa kimapenzi zilianza kusambaa. Miaka mitano baadaye (2012) walipokiri kuwa ni wapenzi.

Hata hivyo, Diddy na Cassie wamekuwa na uhusiano ambao uko mbali na vyombo vya habari na wamekuwa adimu kuonekana pamoja katika matukio yanayowahusisha watu wengi maarufu.

Mara ya mwisho walionekana pamoja wiki tatu zilizopita walipoenda kupata chakula cha usiku, Los Angeles.

Diddy mwenye watoto sita aliowapata katika mahusiano yake ya awali, hivi karibuni alisikika akidai kuwa ana mpango wa kuongeza mtoto mwingine na kwamba angependa azae na Cassie.

Wawili hao hawajasema lolote kuhusu taarifa za kuachana kwao.

Tanzia: Isaac Gamba afariki dunia
Kubenea adai Meya Boniface ndiye ‘wa karibu zaidi’