Benki ya Diamond Trust (DTB) leo imesaini kuingia mkataba na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kudhamini Ligi Kuu Soka Tanzania Bara (VPL) kwa msimu wa mwaka 2016/2017.

DTB inaungana na mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) pamoja na wadhamini wengine katika kudhamini ligi hiyo maarufu kama Ligi Kuu ya Vodacom.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye hafla ya utiaji saini huo iliyofanyika Hoteli ya Serena, Mkuu wa Kitengo cha Fedha wa Benki hiyo, Joseph Mabusi amesema:  “Udhamini huu utasaidia zaidi maendeleo ya soka nchini kwa kuziwezesha timu timu shiriki pamoja na jitihada zingine za TFF. Soka inaunganisha Watanzania wa matabaka mbalimbali ambao ni wateja wetu na si kama benki tungependa kuwa karibu nao zaidi kupitia mchezo huu.”

Mabusi aliongeza kwa kusema:  “Tunafurahi na kujivunia kuwa sehemu ya ligi kuu na tunaamini udhamini huu utazidisha ari ya kuwahudumia Watanzania wote.

Benki ya Diamond Trust imekuwa ikiipa kipaumbele michezo mbalimbali ikiwemo soka, ambapo timu rasmi ya soka inayoundwa na Wafanyakazi imefanikiwa kushinda vikombe na mataji mbalimbali ya soka likiwemo taji la ligi ya mabenki nchini inayojulikana kama BRAZUKA KIBENKI mwaka 2015 pamoja na ngao ya hisani ya ligi hiyo mwaka 2016.

Benki pia inadhamini timu ya soka ya Agathon iliyopo Mbagala inayoshiriki ligi soka daraja la tatu. Zaidi ya hayo benki pia inajivunia kuwa moja kati ya wadhamini wa michuano ya CECAFA Kagame Cup mwaka 2015.

Ligi hiyo inajumuisha timu 16 kutoka Tanzania bara zinazocheza kwa mfumo wa mechi za nyumbani na ugenini ambazo ni Young Africans, Simba Sports Club, Azam FC, Mtibwa Sugar, Kagera Sugar, Mbeya City, Majimaji, MbaoFC, African Lyon, JKT Ruvu, Ruvu Shooting, Tanzania Prisons, Stand United, mwadui FC, Ndanda FC na Toto Africans.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa Shirikisho la Soka Tanznaia –TFF wakiongozwa na Rais wao Ndugu Jamal Malinzi, Wafanyakazi wa Benki ya DTB, wawakilishi kutoka Vodacom, wadau mbalimbali wa soka pamoja na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini.

Malinzi ameshukuru na kuupongeza udhamini huo uliotolewa na benki hiyo na pia ameziomba taasisi nyingine kuiga mfano huo ili kukuza soka nchini. “Kwa heshima ana furaha kubwa nawakaribisha DTB Tanzania kwenye ligi kuu na familia ya TFF kwa ujumla.”

Benki ya Diamond Trust ina matawi 25 nchini, ikiwa na matawi kumi na moja (11) jijini Dar es Salaam (Mtaawa Jamaat, Masaki, Morocco, Magomeni, Mbezi, Mbagala, barabara ya Nyerere, Msimbazi – Kariakoo, barabara ya Nelson Mandela, Upanga katika barabara ya umoja wa mataifa na katika makutano ya barabara ya Mirambo na mtaa wa Samora).

Vile vile ina matawi katika miji ya Arusha (2), Mwanza (2) na katika miji ya Dodoma, Kahama, Mbeya, Morogoro, Moshi, Mtwara, Mwanza, Tabora ,Tanga na Zanzibar.

DTB Tanzania ni mshirika wa mtandao wa maendeleo ya kiuchumi wa Aga Khan – Aga Khan Fund for Economic Development (AKFED) ambao ni sehemu ya mtandao wa maendeleowa Aga Khan Development Network).

DTB Kenya ni miongoni mwa wanahisa muhimu wa DTB Tanzania.

DTB Tanzania pia ni sehemu ya mtandao wa mabenki ya DTB Group yenye matawi zaidi ya 120 Afrika Mashariki na kati.

Waziri Mkuu apokea misaada ya Waathirika tetemeko Kagera
Serengeti Boys Kuweka Kambi Nje Ya Nchi