Mkuu wa wilaya ya Ludewa mkoani Njombe, Andrea Tsere amewataka wadau wa elimu walioko ndani na nje ya wilaya hiyo kukutana ili kuweza kujadili masuala mbalimbali ya kukuza elimu katika wilaya hiyo.

Katika mkutano huo unatarajiwa kufanyika tarehe 20 mwezi huu una lengo la kujadili changamoto mbalimbali za elimu ambazo zimekuwa zikiikumba wilaya hiyo hasa katika miundombinu ya ufundishaji.

Ameyasema hayo wilayani humo wakati akizungumza na Dar24Media, ambapo amesema kuwa mkutano huo utaambatana na harambee ya kuchangia pesa na vifaa mbalimbali vya elimu ili kufufua na kutunisha mfuko wa elimu katika wilaya ya Ludewa, mfuko ambao haufanyi kazi kutokana na kukosa pesa kwaajili ya uendeshaji.

“Tuna kazi ya kukuza kiwango cha ufaulu kwa shule zetu za msingi na sekondari kutoka asilimia 78 mwaka 2018 hadi tuhakikishe tunafikia asilimia 90 ya ufaulu mwaka huu 2019, nilipoteuliwa tu na Rais Magufuli kuwa mkuu wa wilaya hii ya Ludewa niliona hali ya elimu katika wilaya yetu hairidhishi ndipo mwaka jana February 20 niliitisha kongamano la kwanza la elimu kwa wadau wa Ludewa wanaoishi nje ya wilaya hii kisha matokeo yakawa mazuri hivyo nimeona tukutane tena February 20 mwaka huu na tukio hili ni endelevu kila mwaka,” amesema DC Tsere

Kwa upande wao wadau wanaoishi nje ya wilaya ya Ludewa wamesema kuwa kongamano hilo lililoanzishwa na mkuu wa wilaya hiyo ni jambo la kuungwa mkono na kila mwananchi na mdau wa maendeleo wilayani Ludewa kwakuwa Wilaya hiyo bado inahitaji mtokeo chanya ya kuridhisha katika sekta ya elimu.

 

Wananchi wa Kijiji cha Nandete wajitolea kujenga Zahanati
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Februari 10, 2019