Mkuu wa wilaya ya Kilolo, mkoani Iringa, Asia Abdalah amepewa onyo kwa kutumia madaraka yake vibaya na kutokuwa na uhusiano mzuri na watumishi waliopo ofisini kwake kwa kuwafukuza hovyo na wengine kuwaweka mahabusu.

Onyo hilo amepewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katika ziara yake wilayani humo, ikiwa ni mara ya pili kwa Majaliwa kumzungumzia vibaya mkuu huyo wa wilaya, baada ya mwaka 2016 kubainisha mbele ya watumishi wa halmashauri ya Wilaya hiyo kuwa mkuu huyo hana uhusiano mzuri na walio chini yake.

Jana Majaliwa amesema kuwa, Asia amekuwa hana uhusiano mzuri na wtumishi wake na imefikia mahali watumishi wanaogopa hawana raha na wengine wameamua kuhamia Wilaya nyingine na hata waliopo hawataki kuendelea kufanya kazi naye.

Amesema, kutokana na kutoelewana na watumishi walio chini yake, hadi sasa amebadilisha madereva 10 tangu alipoteuliwa kuwa mkuu wa Wilaya hiyo, jambo linalofanya ajiulize kama kweli wote hawana sifa ya kumuendesha au wana matatizo.

“Mkuu wa wilaya ni vyema ukakaa vizuri na watumishi wako, ofisi yako watumshi wanahama sana na sina uhakika kama wote hawana matatizo, kwani mtu yeyote anapopata barua na kuambiwa anakwenda kilolo kufanya kazi ofisi ya mkuu wa Wilaya anaanza kukata tamaa Alisema Majaliwa” Alisema Majaliwa.

Amesema mbali na kuwafukuza madereva 10 hadi sasa, DC huyo hajaelewani na wasaidizi wake wengine kama katibu tawala ambaye anapaswa kufanya naye kazi kwa ukaribu.

Na kumtaka katibu tawala mkoa asitoe fedha za uhamisho kwa mtumishi kumpeleka Kilolo, waliopo wabaki na kama hawafai mkuu wa wilaya atoe ushauri ili wafukuzwe kazi kabisa.

” Haiwezekani ofisi ya mkuu wa Wilaya ikawaondoa watumishi wote, haiwezekani kuna shida, mkuu wa mkoa rudi hapa Kilolo na chukua hatua zaidi, hii ya  DC kubadili madereva 10 ni mpya na haijawahi kutokea. watumishi wake wanakwenda ndani?” aleongeza Majaliwa.

Na kusisitiza kuwa viongozi watumie dhamana za uongozi kwa maslahi ya wote kwa weledi mkubwa, umoja na mshikamano ndio nguvu yao kubwa.

Hata hivyo mkuu huyo wa wilaya aliomba radhi kwa kujitetea kuwa yeye si malaika hivyo ataendelea kuwa mtiifu nje na ndani ya uongozi na hata atakapo ingia kaburini.

” Inawezekana tunafanya mazuri na mengine tunafanya mabaya, lakini hata mtoto akikuudhi basi kuna nafasi pia ya kumsamehe, mimi ni kiongozi mtiifu nitaendelea kuwa mtiiifu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nje ya uongozi na ndani ya uongozi na hata nikiingia kaburini. kwahiyo mimi sio malaika naomba unisamehe” alisema Asia

 

 

Video: Serikali yawaonya wanaobeza elimu ya watu wazima.
Tanazania yavunja rekodi ya Uganda 'JAMAFEST'