mkuu wa wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe, Ally Kassinge ameonesha kusikitishwa na kitendo cha wilaya yake kushika nafasi ya mwisho kimkoa katika uhamasishaji wananchi kujiunga na mfuko wa bima ya afya CHF iliyoboreshwa, hatua ambayo inapaswa kufanyiwa kazi kwa kila mhusika.

Katika kikao cha baraza la madiwani halmashauri ya wilaya ya Wanging’ombe, mkuu wa wilaya hiyo amesema tangu kuzinduliwa kwa bima ya afya CHF iliyoboreshwa wiki chache zilizopita na mkuu wa mkoa wa Njombe, Christopher Ole Sendeka, bado halmashauri hiyo imeonekana kuburuza mkia kati ya halmashauri sita za mkoa wa Njombe jambo ambalo halikubaliki.

“Tathmini ya CHF iliyoboreshwa tangu kuzinduliwa kwake wiki tatu zilizopita na mh.Mkuu wa mkoa halmashauri yetu kwa masikitiko sana ni ya mwisho, mganga mkuu tunaye,waratibu tunao, watendaji tunao na wataalamu wa hizo kazi tunao lakini kati ya malengo tumeandikisha sijui 280 ,hatujafanya vizuri lakini tuna kazi ya ziada ya kuelimisha watu wetu” amesema Kassinge

Antony Mahwata ni mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Wanging’ombe amekiri kupokea maelekezo hayo na kumuagiza mkurugenzi na wataalamu wake wa afya kuhakikisha wanashirikiana na madiwani kuwahamasisha wananchi kujiunga na bima hiyo.

“Nina imani kwamba watu wakihamasishwa kuhusiana na CHF iliyoboreshwa kwasababu ni faida kwao watajitokeza, niseme tunajiskia aibu sana kutokana na jambo hili kwa hiyo nitoa rai ndugu zangu Wanging’ombe tubadilike” alisema Mahwata

Baadhi ya madiwani akiwemo Fredrick Mwalongo kutoka kata ya Wangama wamesema wanahitaji kuelimishwa zaidi juu ya CHF iliyoboreshwa kwani wanashindwa kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi kwa kuwa nao hawana uelewa wa kutosha.

Bima ya afya iliyoboreshwa imetoa uwanja mpana wa huduma hadi hospitali za rufaa za mikoa kwa shilingi elfu 30 tofauti na hapo awali.

Chukua haya unapomtembelea mama aliyejifungua, ''Using'ang'anie kubeba mtoto''
Mtoto aishi miaka 12 na jiwe puani