Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amewataka wananchi wa mkoa huo kujitokeza kwa wingi katika viwanja vya Zakheim Mbagala kwa ajili ya kusajili laini zao za simu, ikiwa imebaki siku moja na saa kadhaa kufikia ukomo wa usajili wa laini kwa alama za vidole.

Makonda ametoa wito huo kupitia kipande cha video ambacho kimesambazwa mtandaoni ambapo ameeleza kuwa takribani wakaazi wa mkoa huo milioni 7 wenye namba za Vitambulisho vya Taifa (NIDA) hawajasajili laini zao.

“Takwimu nilizonazo watu milioni saba wenye namba na vitambulisho vya NIDA hawajasajili laini zao. Habari njema kwa wakaazi wa Dar es Salaam, tumeandaa eneo hili [Zakheim Mbagala] kwa ajili ya kuwapa fursa kusajili laini zao,” amesema RC Makonda.

“Kampuni zote za simu zitakuwepo. Simu ni yako na laini ya kwako na Tanzania ni Taifa lako, kwa nini usitumie fursa hii kukamilisha mchakato huu utakaolinda usalama wa mali zako na Taifa,” aliongeza.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli aliongeza siku 20 za usajili wa laini za simu, kutoka Desemba 31 mwaka 2019 iliyokuwa imetangazwa na Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) na alisisitiza kuwa baada ya hapo laini ambazo hazijasajiliwa zitazimwa.

Tumia hivi ndizi kwa urembo wa uso
Zijue faida za vitamini A mwilini