Makamu Mwenyekiti wa Young Africans, Frederick Mwakalebela, amepinga azimio la Kamati ya Uongozi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara la kusitisha shughuli zote za michezo kwa mwezi mmoja ili kudhibiti maambukizi ya visusi vya Corona.

Kamati ya Uongozi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara, ilikutana Jumanne wiki hii kwenye kikao cha Dharura kilichoitishwa na Rais wa TFF Wallace Karia, kwa lengo la kujadili mustakabali wa ligi kutokana na mlipuko wa virusi vya ugonjwa wa Corona ambao umeingia nchini.

Mwakalebela, alisema uamuzi uliotangazwa na Bodi ya Ligi si sahihi na si suluhisho kwa tishio lililopo la ugonjwa huo ambao unaisumbua dunia kwa sasa.

Mwakalebela aliongeza kuwa TFF na vyombo vyake inapaswa kuwa na subira kwa sababu endapo virusi vya corona vitaendelea kuwapo, itakuwa vigumu kudhibiti mkusanyiko wa mashabiki kwenye ‘vibanda umiza’ ambavyo vimeenea katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

“Bado haitakuwa suluhisho, mkusanyiko wa watu utaendelea kuwapo, hatuna uwezo wa kudhibiti katika maeneo mbalimbali nchini ambayo yatakusanya mashabiki, ni bora tusubiri janga limalizike, huko duniani (nchi zilizoendelea), wameona haina tija, iweje sisi tucheze,” Mwakalebela alisema.

Maazimio mengine yaliyofikiwa kwenye kikao cha Kamati ya Uongozi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Golden Tulip Jijini Dar es Salaam Jumanne, wachezaji wote walamika kupimwa virusi vya Corona kabla ya kuendelea na mechi.

Azimio la tatu, michezo itachezwa bila ya mashabiki baada ya siku 30 za kusimamishwa kwa mashindano yote nchini katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa Corona ulioingia nchini.

Aidha, Bodi imeazimia kuwa ligi imalizike ndani ya mwezi Juni ili kutoa nafasi kwa timu zitakazoiwakilisha nchi kimataifa kuendelea na mchakato wa mashindano ya CAF lakini pia bodi itaendelea kusimamia afya kipindi hiki cha tahadhari ya Corona.

Corona: Zanzibar yazuia safari za watalii
Yondani atunisha msuli Young Africans