Jana Ijumaa, waziri wa Afya, Mutahi Kagwe alitangaza kisa cha kwanza cha mgonjwa wa Corona nchini humo ambaye alithibitika siku ya Alhamisi usiku.

Baada ya tangazo hilo, raia walionekana wakikimbilia kwenye maduka ya jumla kununua kemikali za kuua viini vya bakteria mikononi maarufu kwa kiingereza kama ”hand sanitisers” pamoja na barakoa za kufunika uso.

Imeelezwa kuwa wateja walioanza kumiminika nyakati za mchana walikuwa na wakati mgumu kupata bidhaa hizo zilizokuwa adimu ghafla za kemikali za kunawa mikono zinazoua viini mara moja na barakoa.

Baadhi ya wateja walilazimika kununua bidhaa nyingine mbadala za kuua viini mfano wa zile zinazotumika wakati wa kuosha nguo mara nyingi ikiwa ni zile za watoto wadogo, lakini wakati huu zikilengwa kumimininwa kwa kaisi kidogo katika maji ya kunawa mikono au kuosha sakafu.

Licha ya kwamba, maduka ya jumla na yale ya kuuza dawa yameahidi upatikanaji wa bidhaa hiyo kwa kiwango kikubwa, baadhi ya wateja wanahofia kwamba huenda bei za bidhaa hizo ikapanda maradufu kwasababu ya uhitaji wake wakati huu.

Serikali ya kenya imefahamisha raia kwamba hakuna haja ya kuwa na hofu licha ya kuthibitishwa kwa kisa cha kwanza cha mgonjwa wa Corona.

Mahakama: Msigwa alitoka kwa faini ya Magufuli
Video: Magufuli atishwa na kasi ya Corona, Sekeseke la Chadema Segerea