Mwenyekiti wa Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA), Hashimu Rungwe, amesema kuwa chama chake hakitashiriki uchaguzi wa Serikali za mitaa utako fanyika Novemba 24 mwaka huu.

Hapo awali, Novemba 7 Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kilitangaza rasmi kutoshiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, siku ya Novemba 24, ambapo pia kiliwataka wagombea wake walioenguliwa kutokata rufaa.

Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe alitangaza uamuzi huo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, baada ya kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho kufanyika, ambapo alidai hawakubaliani na sababu za wagombea wa chama hicho kukatwa.

Jana Novemba 8, Kiongozi wa Chama cha ACT – Wazalendo, Zitto Kabwe, alitangaza kuwa chama hicho hakitoweza kushiriki tena Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, kwa kile alichokieleza kuwa wagombea wao zaidi la Laki moja, wameenguliwa na kubaki na wagombea Elfu 6 pekee, sawa na asilimia 4 ya wagombea wote.

“Sisi hatutashiriki kwa sababu tumeondolewa, toka juzi tumekuwa na mashauriano na vyama vya siasa nchini, wenzetu wametoa maamuzi yao jana, sisi tumetoa maamuzi yetu leo, tutawajulisha wananchi hatua gani tutaenda kuchukua kwa ajili ya kulinda kilicho chetu, wao wametuondoa asilimia 96 na sisi tumewasaidia kuiondoa ile asilimia 4 ili tusishiriki kabisa” alisema Zitto.

Ikumbukwe kuwa jana, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, alikionya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kuhusiana na msimamo wake wa kujitoa kwenye zoezi la Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa madai ya kwamba, anadhani mpango huo huenda ukawa na nia ya kuchafua amani.

Na katika hatua nyingine Leo, Waziri wa TAMISEMI, Seleiman Jafo amesema kuwa kwamujibu wa kanuni za uchaguzi jina la mgombea likishateuliwa linabaki kwenye karatasi za kupigia kura siku ya uchaguzi hata kama chama chake kimejiengua kushiriki kwenye uchaguzi.

Wizkid, Tiwa savege kwenye ardhi ya Tanzania
Alikiba amjibu shabiki wa Diamond aliyerudisha Penseli