Mabingwa watetezi Cameroon na wenyeji Misri wameyaaga mashindano baada ya kutolewa kwenye siku ya pili ya hatua ya mtoano.

Cameroon na Misri ndio waliocheza fainali ya Kombe la Maifa ya Afrika (Afcon) miaka miwili iliyopita ambapo Cameroon ilitwaa ubingwa.

Timu hizo mbili zimeyaaga mashindano baada ya Cameroon kufungwa 3-2 dhidi ya Nigeria jijini Alexandria, huku Misri wakipigwa mbele ya mashabiki elfu sabini jijini Cairo na Afrika Kusini kwa goli moja tu lililofungwa na Thembinkosi Lorch katika dakika ya 85.

Afrika Kusini ambao walifuzu katika raundi ya mtoano kama timu ya tatu kwenye kundi lao baada ya kushinda mchezo mmoja tu haikupewa nafasi kubwa katika mechi dhidi ya Misri inayoongozwa na mshambuliaji wa Liverpool Mo Salah.

Aidha, Umakini wa safu ya ulinzi wa Afrika Kusini ndio imekuwa chachu ya ushindi baada ya kuhimili vishindo na mikiki ya safu ya ushambuliaji ya Misri ambayo iliibuka na ushindi kwenye mechi zote tatu za makundi.

Katika mechi ya Nigeria na Cameroon, Nigeria walifanikiwa kuwavua ubingwa mabingwa watetezi Cameroon kwa kuwachapa goli 3-2 na kuwaondosha katika mashindano hayo ambayo yamekuwa na mvuto mkubwa.

Nigeria ilianza kwa kasi katika mchezo huo na kutangulia kupata goli katika dakika ya 19 kupitia Odion Ighalo. Cameroon wakajibu mapigo kama Simba aliyejeruhiwa na kupata magoli mawili ya haraka kupitia Stephane Bahoken na Clinton N’Jie.

Katika kipindi cha pili, Nigeria ikarudi kumaliza mchezo. Ighalo alipachika goli la kusawazisha katika dakika ya 63 na dakika tatu baadaye, Ighalo akamtengea Alex Iwobi pasi safi aliyoiunganisha na kupachika bao la ushindi kwa Nigeria

Deni la Bil. 1 lazidi kumtafuna Mbowe, mali zake zapigwa mnada
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Julai 7, 2019