Askofu wa Kanisa la Ufufuko na Uzima, Josephat Gwajima jana alijibu tuhuma za aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Wilbroad Slaa ambaye siku chache zilizopita alimtaja askofu huyo kama mshenga aliyempeleka Edward Lowassa katika chama hicho.

Katika hotuba yake, Dk Slaa alimtaja askofu huyo kuwa ndiye aliyemwambia kuwa maaskofu 30 kati ya 34 wa kanisa katoliki walihongwa fedha na Edward Lowassa.

Akiongea na waandishi wa habari, Gwajima alijibu mapigo kwa kueleza siri nyingi kati ya wawili hao huku akidai kuwa Dk Slaa ni muongo na kwamba aliudanganya umma kwa shinikizo la mkewe aliyenunuliwa na maadui wa Chadema. Alisema mkewe huyo tayari alikuwa amejiandaa kuwa ‘first lady’ na hakutaka kupoteza nafasi hiyo.

Pamoja na mambo mengine, Gwajima alieleza kuwa Dk Slaa aliudanganya umma kuwa sababu za yeye kuachana na siasa ni ujio wa Edward Lowassa ndani ya Chadema iliyokuwa ikipinga ufisadi. Alidai kuwa Dk Slaa ambaye alikiri ni rafiki yake, ndiye aliyemfuata na kumshawishi ampeleke Lowassa Chadema ili awezeshe chama hicho kushinda katika uchaguzi mkuu.

“Dk. Slaa alikuja kwangu nimuunganishe na rafiki yangu Lowassa kwa sababu ni mtu mwenye mvuto katika chama chake, jamii na ana nguvu kisiasa. Mimi nataka nikiri kwamba nilifanya kila linawezekana ili kuhakikisha Lowassa anakwenda Chadema,” alisema.

“Dk. Slaa alivyoniita Mshenga hakukosea kwa sababu ninajua kila kitu. Mimi kusaidia kumleta Lowassa Chadema ni kazi ya Mungu, maana Biblia inasema ‘heri wapatanishi maana hao wataitwa wana wa Mungu’.” Aliongeza.

Gwajima alieleza kuwa Dk Slaa alikuwa na nia ya kumpeleka Lowassa Chadema akiwa kama Katibu Mkuu wa Chama na kwamba ndiye aliyemkutanisha na mwenyekiti wa chama hicho na mwisho kuingia katika kamati kuu ambapo alipokelewa vizuri na wananchama wa chama hicho baada ya kuhutubia.

Alisema hata hivyo mke wa Dk Slaa, Josephin aligeuka kikwazo kikubwa baada na kuanzisha ugomvi akimtaka kubadili mawazo yake, huku akisimulia tukio la kutupiwa begi nje na mkewe na kulazimika kulala kwenye gari lake.

Gwajima alisema walinzi wa Dk Slaa ambao alipewa na askofu huyo miaka mitano iliyopita ndio walimfahamisha kuhusu tukio hilo la kulazwa nje. Pia, Dk. Slaa alimtumia ujumbe ambao aliuonesha kwa vyombo vya habari, ujumbe uliokuwa ukieleza kuwa Dk Slaa anataka kuachana na siasa kwa kuwa familia yake inapasuka.

Katika hatua nyingine, Gwajima amemuelezea mke wa Dk Slaa kuwa ni mtu mwenye mashetani na mara nyingi amekuwa akimuombea na kwamba ameibadili akili ya Dk Slaa na kusema hayo anayoyasema leo. Alisisitiza kuwa kinachoongea sio akili ya Dk Slaa, bali anaendeshwa na mkewe.

Aidha, alikanusha kauli ya Dk Slaa kuwa alimwambia maaskofu walihongwa na wakagawana fedha mbele ya macho yake. Alimtaka kuacha mara moja kuwahusisha maaskofu na siasa kwa kuwa anachokizungumza sio kweli na kwamba anapaswa kuacha uongo unaowachafua maaskofu ili kumridhisha mtu au chama kilichomtuma.

Baada ya maelezo marefu, Gwajima alimuonya Dk Slaa kutorudia kumtaja kwa kuwa siri zake zote anazifahamu na kwamba alikuwa anarekodi maongezi yao.

“Nasema kama Dk. Slaa atajaribu kujibu haya, nitatoa siri nzito namna alivyokwenda Afrika Kusini akiwa na wanne wanne pamoja na mzigo uliopo na mahali ulipotunzwa,” alisema.

Wakati Gwajima anatoa maelezo hayo, taarifa zinaeleza kuwa Dk. Wilbroad Slaa amesafiri na familia yake kuelekea nchini Marekani. Hata hivyo, Dk Slaa ameiambia Azam TV kuwa ameondoka nchini sio kwa kukimbia bali ameenda kwa ajili ya mapumzika na atakuwa akifuatilia kinachoendelea nchini.

Haijafahamika kama bomu hilo la Gwajima limepokelewaje na Dk Slaa, na kama atajitokeza tena kujibu huku kukiwa na onyo la askofu huyo ambaye amewataka maaskofu wote kutohangaika na tuhuma za Dk Slaa kwa kuwa yeye atammudu.

 

 

Dk Slaa Afunguka Tena
Serena Williams Amtesa Tena Ndugu Yake