Shirikisho la ngumi Tanzania (BFT) limesikitishwa sana na moja ya gazeti la michezo la hapa nchini lililoandika habari zenye lengo la kudhoofisha jitihada zinazofanywa na shirikisho kwa kusaidiana kwa karibu na serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa waziri mwenye dhamana ya michezo Mh. Harrison Mwakyembe.

Gazeti hilo kupitia kwa mwandishi wake ambaye siku zote amekuwa akiandika habari zenye mlengo wa kubomoa pale njia inapoanza kuonekana aliandika kuwa timu taifa ya ngumi inaishi kwa kunywa chai na chapatti mbili na tuhuma nyingine za kukejeri timu hiyo,,kitu ambacho shirikisho linakanusha kuwa si kweli.

Kwa hali ya kawaida tu binadamu yeyote hawezi akaishi kwa kunywa chai na chapati mbili akamudu kufanya mazoezi magumu ya mchezo wa ngumi kutwa mara tatu.

Ukweli uliopo ni kuwa timu yetu ya taifa ya ngumi ipo katika maandalizi ya kwenda kuwakilisha taifa katika mashindano ya jumuiya ya madola yatakayofanyika kuanzia tarehe 04-15 Aprili 2018 Nchini Australia.

Timu hiyo ipo katika mazoezi yanayoendelea kila siku uwanja wa taifa wa ndani kwa mtindo wa kwenda mazoezini na kurudi majumbani kwao hadi mwezi mmoja kabla ya mashindano ndio tunategemea kuwaweka katika kambi ya pamoja kwa maandalizi ya mwisho.

Kwa hivi sasa wachezaji hao ambao wengi ni watumishi wa umma wanapata mahitaji yao ya msingi kutoka kwa waajili wao hadi hapo watakapokuwa katika kambi ya pamoja, ingawa kumekuwa na msaada wa kuboresha pale inapowezekana..

Awali Shirikisho kwa kushirikiana na Serkali na TOC waulikuwa na mpango wa kuwapeleka katika kambi ya mazoezi nchini Cuba lakini mpango huo haukukamilika.

Timu hiyo kwa sasa ina jumla ya mabondia wanaume, kumi na watatu miongoni mwao ndio watawakilisha taifa katika mashindano hayo lakini pia kuna mabondia kumi wanawake wakifanya mazoezi pamoja nao.

Aidha shirikisho la ngumi Tanzania baada ya kupata habari hizi imeona si busara kukaa kimyaa kwa habari kama hizi na kuchukua hatua ya kukanusha kwa nguvu zote na kuwaomba waandishi wa habari kutokuandika habari ambazo hazina ukweli na hazina faida kwa maendeleo ya nchi.

Kwa mfano kwa hivi sasa mabondia hao wa timu ya taifa wapo katika maandalizi ya kwenda kuwakilisha taifa la Tanzania katika mashindano ya jumuiya ya madola. Tunachokiomba waandishi ni Kuandika ukweli uliopo wenye kuwajenga kisaikolojia ili watangulize utaifa mbele na hatimaye uwakilishi wa timu zetu za taifa uwe wenye tija.

Na sio kuandika habari za uchochezi na udhalilishaji kwa wachezaji wetu kwa nia ya kukosanisha mabondia na uongozi au shirikisho na serikali.

Serikali kwa kipindi hiki imekuwa karibu sana kuhakikisha changamoto zote zinazotukabili zinaondolewa lakini zaidi hata uwanja wa taifa wa ndani tunaofanyia mazoezi tumepewa na serikali.

Wasira awapiga dongo wapinzani
Kamati ya saa 72 yasikiliza malalamiko ya Dodoma FC