Baraza la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA), Wilaya ya Shinyanga Mjini, limelitaka Jeshi la Polisi kutoingilia uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu.

Hayo yamesemwa mkoani Shinyanga na Mwenyekiti wa BAVICHA wa wilaya, Samson Ng’wagi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ambapo ameliomba jeshi hilo kuviacha vyama vya siasa vishindane kwa hoja.

Amesema kuwa kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na ule wa marudio katika kata na majimbo mbalimbali, jeshi hilo lilikuwa likiingilia uchaguzi huo mara kwa mara.

“Tunaliomba Jeshi la Polisi lisitumike kisiasa na kukipendelea chama tawala bali lifanye kazi yake ya kulinda amani na lisiwe sehemu ya chanzo cha vurugu. lituache sisi wanasiasa tushindane kwa hoja majukwaani,” amesema Ng’wagi.

Hata hivyo, Mwenyekiti huyo ameongeza kuwa, wao CHADEMA huwa wanachukizwa sana pale wanapoliona jeshi la polisi ambalo ndiyo wanalitegemea kulinda usalama wa raia kuwa sehemu ya wanasiasa.

 

Video: Sababu ya wanawake wa kabila hili kutoboa midomo na kuweka visahani
Davido, J Cole kupanda jukwaa moja katika tamasha la DreamvilleFestival