Baraza la Kijeshi na viongozi wa upinzani nchini Sudan, wamesaini makubaliano ya kugawana madaraka mara baada ya mazungumzo ya usiku kucha kumaliza mzozo nchini humo.

Makubaliano hayo ya miaka mitatu ya uongozi wa pamoja utakaofuatiwa na uchaguzi mkuu, ambao utaamua hatma ya nchi hiyo ambayo iliingia katika machafuko siku za hivi karibuni.

Baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, viongozi wa pande zote wamezungumzia kizazi kipya katika taifa ambalo limeshuhudia ghasia na mauaji ya mamia ya waandamanaji tangu kutimuliwa kwa kiongozi aliyekuwepo madarakani, Omar Al Bashir mnamo Aprili mwaka huu.

Katika makabiliano na jeshi yaliyogeuka kuwa ghasia zilizosababisha vifo vya mamia ya watu, waandamanaji walitaka jeshi likabidhi madaraka kwa utawala wa kiraia.

Aidha, utiaji saini wa makubaliano hayo, unaonekana kuthibitisha makubaliano yaliyo idhinishwa kimsingi mapema mwezi huu, ambapo yanaeleza kuwa jeshi litakuwa madarakani kwa kipindi cha miezi 21 ya kwanza, na baada ya hapo utawala wa kiraia utaidhinishwa katika miezi 18 itakayofuata, na kufuatiwa kufanyika kwa uchaguzi mkuu.

Hata hivyo, makubaliano ya pili kuhusu masuala ya katiba yanatarajiwa kukamilishwa Ijumaa wiki hii.

Unai Emery: Arsenal inahitaji wachezaji wa bei kali
Kanyasu awang'ata sikio wakulima wa Pamba, 'Msiwauzie walanguzi'