Kocha zamani wa Yanga,  Mwinyi Zahera huenda  akarejea tena kufundisha kwenye moja ya vilabu vikubwa vinavyoshiriki Ligi kuu Tanzania bara.

Zahera ametoa kauli hiyo baada ya siku chache tangu atimuliwe Yanga kwa kile kilichotajwa matokeo mabaya ya timu hiyo ikiwemo kuondolewa kwenye kombe la Shirikisho Afrika.

Juzi usiku, kocha huyo alitarajiwa kusafiri kuelekea DR Congo, kwa ajili ya kujiunga na timu ya taifa ya nchi hiyo inayojiandaa na michezo ya kirafiki.

Akizungumza na moja ya chombo cha habari kilichopo nchini, Zahera alisema yupo tayari kurejea Tanzania kuja kuzifundisha timu kubwa zenye malengo ya kuchukua ubingwa na siyo kushiriki ligi kuu pekee.

Zahera alisema zipo baadhi ya timu kama KMC, Kagera Sugar, Mtibwa Sugar na Mbao FC zenyewe hazifikirii ubingwa zaidi ya kushiriki, hivyo atarejea Tanzania kufundisha kati ya Simba, Azam FC na Yanga aliyoachana nayo.

Aidha, kocha huyo amewataja wachezaji wake bora katika ligi kuu kuwa ni John Bocco anayekipiga Simba na Aggrey Moris wa Azam huku akikataa kuwataja wachezaji aliokuwa akiwanoa kama Kelvin Yondani.

“Mimi ni kocha, hivyo ni ngumu kusema kuwa sitarejea tena kufundisha soka baada ya kuachana na Yanga, nikwambie tu ipo siku nitakuja tena kufundisha moja ya klabu kubwa hapa Tanzania” Amesema Zahera

Na kuongeza “Ninazitaka klabu hizo kubwa kutokana na malengo yao ya kutaka kuchukua mataji ikiwemo wa ligi ili tupate nafasi ya kucheza michuano ya kimataifa Afrika”

“Ni ngumu kwangu kwenda kwenye timu ndogo kama Mbao, KMC, Mtibwa Sugar na Kagera Sugar ambazo zenyewe zimejiwekea nafasi yao katika ligi ambayo ni nafasi ya nne kwenda chini, hivyo basi niahidi kurejea tena nchini hata kama siyo Yanga,” alisisitiza Zahera.

Wizkid aweka wazi mradi mpya atakaoufanya Tanzania wiki hii
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Novemba 10, 2019