Mabingwa wa Kombe La Shirikisho Tanzania Bara (ASFC) Azam FC wamepeana mkono wa kwaheri na Mshambuliaji kutoka nchini Zimbabwe Donald Ngoma. Ilitabirika kirahisi jinsi mwisho wao utakavyokuwa kutokana na maisha ya Ngoma ndani ya timu.

Muda mwingi Ngoma alikuwa akishinda katika vitanda vya Hospital kujiuguza, muda mwingine tulikaa nae jukwaani. Ni mara chache alizovaa jezi ya Azam fc na kuitumikia. Ni kama alikuwa mtumishi hewa pale kwenye viunga vya Chamazi. Kilichotokea leo kilikuwa rahisi kukitabiri. Muda tu, ulikuwa haujafika. Leo yametimia.

Ngoma wa Azam fc ni tofauti na Ngoma wa Yanga. Ngoma wa Yanga alikuwa Ngoma kweli. Alitengeneza presha kwa mabeki kiwanjani hadi mashabiki jukwaani. Ngoma alikuwa mwanaume kweli. Ni Bull striker.

Yanga iliumia Ngoma kuondoka. Alisajiliwa Azam fc akiwa Hospital na magongo yake. Manazi wa Yanga waliumia walipoona rafiki yangu Popat amesimama na Ngoma akimtambulisha kama mchezaji wao mpya.

Usajili wake Azam fc ulikuwa usajili mwingine uliokwenda kuchoma choma mioyo ya mashabiki wa Yanga. Ni kama ilivyokuwa kwa Frank Domayo alipoondoka kujiunga Azam fc. Ngoma lilikuwa kombola lingine kali kutokea Chamazi lililotumwa Jangwani.

Aliwahi kuniambia moja ya rafiki yangu mmoja mchezaji wa Simba nyakati zile ambazo Ngoma alikuwa mchezaji wa Yanga. Aliniambia “Ngoma alikuwa akitupa wakati mgumu tulipokuwa tunajiandaa dhidi yao. Alikuwa anatupa presha kiwanjani. Alikuwa mtemi, muhuni na mgumu kiwanjani. Sio mshambuliaji mwepesi mwepesi kumzuia”.

Leo hii rafiki yangu yule ameshituka na taarifa za Ngoma kupewa mkono wa kwaheri na Azam fc. Amesikitika, lakini jambo moja nililomwambia ni kwamba Ngoma aliuacha mpira Yanga, Azam fc lilienda jina lale.

Ngoma anayefunga bao, kisha anamshika kolodani beki wa adui na baadae kumkolomea mwamuzi angewezaje kuachwa Azam Fc kama kaachwa Gaudence Mwaikimba? Ngoma yule alikuwa wa moto. Alitamaniwa na kila timu. Azam fc nyakati zile ingekuwa ngumu kumpata na kumleta Chamazi. Ingewezekana vipi?

Ngoma alikamilika. Lakini tukubaliane na Azam Fc walioachana nae. Hawajamuacha kimizengwe. Namba hazidanganyi. Anyway Ngoma wasalimie huko Zimbabwe. Tutakukumbuka kwa yote ndani ya ardhi yetu

Messi afungua ukurasa mpya La Liga
Ajira: Makampuni 10 yatangaza nafasi za kazi, ziko hapa