Hatimaye Antony Joshua ameweka wazi tarehe ambayo amepanga kuzichapa na hasimu wake wa muda mrefu, Deontay Wilder akisisitiza kuwa ni lazima pambano hilo lifanyike nchini Uingereza.

Mbabe huyo ambaye hajawahi kupigwa ameeleza kuwa tayari ameshalipia uwanja wa mpira wa miguu wa Wembley jijini London kwa pambano la Aprili 13 mwakani akimlenga zaidi Wilder.

“Niko tayari kupambana na Deontay Wilder Aprili mwakani jijini London. Sijajua ninapaswa kufanya nini zaidi ili huu ujumbe ufike duniani kote. Yeye naona anachotaka ni kupigana na Tyson Fury wakati Tyson hana mkanda wowote wa ubingwa wa masumbwi wa dunia,” Joshua aliiambia ESPN.

“Nimeshalipia uwanja tayari kabla ya siku. Nimeshalipia hadi tarehe ya pambano, na niweke jambo hili sawa, ninataka kupamba na mtu yeyote hususan Deontay Wilder kwa sababu ni bingwa,” aliongeza.

Alifafanua kuwa asingependa kupigana na Tyson Fury kwa sababu sio bingwa, angependa kupigana na bingwa mwenzake.

Anthony Joshua ana historia nzuri ya kutopoteza pambano kati ya mapambano yake yote 22, na ameshinda kwa KO katika mapambano 21. Vilevile, Deontay Wilder ana rekodi ya kushinda mapambano 40 na kutoa sare pambano Moja, huku akishinda 39 kwa KO.

Wilder ambaye amekuwa akitangaza kuwa na kiu ya kupambana na Joshua, anatakiwa kupigana tena na Fury ili kuondoa utata wa sare kati yao na kumpata mbabe zaidi.

Theresa May awapigia goti viongozi wa EU
Moyo wa binadamu wazua taharuki ndani ya Ndege