Ali Kiba amewashukia watu aliodai anahisi walikuwa wamejipanga kudukua akaunti yake ya YouTube ili kuhakikisha wanamrudisha nyuma asiweke rekodi nyingine kwenye mtandao huo.

King Kiba ambaye video yake ya ‘Mvumo wa Radi’ ilijikuta ikidumaa kwa zaidi ya saa 20 huku idadi ya walioitazama ikiwa inapanda na kushuka, amesema kuwa anaamini waliofanya hivyo watakuwa wametumwa, wamelipwa au wana ni mbaya, lakini hawawezi kumuathiri kiasi walichodhani.

“Kama kuna watu wanafanya figisu na vitu kama hivyo, huo ni utoto. Kwasababu haina maana kufanya vitu kama hivyo,” alisema Ali na kusisitiza kuwa hategemei malipo ya idadi ya watakaoangalia video yake YouTube.

King Kiba aliendelea kufunguka jana kupitia the Playlist ya 100.5 Times Fm kuwa anachoridhika nacho hivi sasa ni jinsi ambavyo watu wameendelea kufurahia muziki wake mzuri hata kama tarakimu hazionekani ipasavyo kwenye YouTube.

“Cha msingi Ommy [Lil Ommy], sisi tunachotaka ni watu kuenjoy muziki mzuri. As long as watu wanapata ujumbe sisi kwetu tuko sawa,” alisema.

Hata hivyo, Kiba amesema kuwa menejimenti yake imefanya mawasiliano ya moja kwa moja na YouTube na kwamba ingawa hawakuwa na jibu la moja kwa moja, anaamini wana kila uwezo wa kurejesha akaunti hiyo kwenye hali salama.

Aidha, kwa mujibu wa mwimbaji huyo, uongozi wa RockStar Africa umejiimarisha kuhakikisha inaongeza ulinzi zaidi katika akaunti zake za YouTube kwa njia za kiteknolojia ili kuhakikisha hali hii haiendelei kuwasumbua.

Video ya Mvumo wa Radi, pamoja na hekaheka ilizokutana nazo, imefanikiwa kufikisha ‘Views’ 1.1 milioni hadi leo. Huenda akaunti hiyo sasa imerudi kwenye mazingira salama.

 

 

 

Sethi wa IPTL avuliwa madaraka
Marekani yafungua rasmi ubalozi wake Jerusalem