Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imemuhukumu kunyongwa hadi kufa Masamba Musiba (39) aliyepatikana na hatia ya mauaji katika kesi ya kumuua mpenzi wake, Betha Mwarabu katika hosteli za Mabibo jijini Dar es Salaam.

Mshitakiwa pamoja na Betha walikuwa ni wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na wakiishi katika hosteli hizo.

Mauaji hayo yalitokea Juni 6, 2009 katika hosteli hizo zilizoko Wilaya ya Kinondoni saa tatu usiku katika hosteli hizo, mshitakiwa alikwenda katika chumba namba 250 cha mpenzi wake ambaye sasa ni marehemu Betha.

Mshitakiwa aliongea na mpenzi wake huyo na ghafla alitoa kisu na kuanza kumchoma kifuani, alianguka chini na baadaye alisaidiwa na wanafunzi wenzake baada ya kusikia akipiga kelele, mshitakiwa alikimbia.

Akitoa hukumu hiyo juzi, Jaji wa Mahakama Kuu, Elvin Mugeta alisema mahakama imefikia uamuzi huo baada ya kukubaliana na ushahidi uliotolewa upande wa mashitaka bila kuacha shaka yoyote, ambako alisema pia hakuona sababu ya mshitakiwa kusingiziwa shitaka hilo.

“Mashahidi waliomuona kwenye tukio walimtambua vizuri na hawakuwa na sababu yoyote ya kumsingizia, kwa hiyo Mahakama inamuona mshitakiwa ana hatia ya mauaji ya kukusudia na hivyo inamhukumu kunyongwa hadi kufa,” alisema Jaji Mugeta katika uamuzi wake.

Ramaphosa akemea mashambulizi dhidi ya raia wa kigeni Afrika Kusini
Ridhiwani Kikwete atoboa siri ya CCM kupendwa na wananchi